BIOTEKNOLOJIA NA UMWAGILIAJI KUPAISHA KILIMO TANZANIA
Rais wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan na Waziri wa Kilimo Hussein Bashe wakivuta pazia kuashiria uzinduzi wa Maabara ya Rufaa ya Taifa ya Kilimo Agosti 8, 2025 iliyopo Mtumba Jijini Dodoma.
Na Dotto Mwaibale
Katika historia ya maendeleo ya kilimo nchini Tanzania,
Agosti 8, 2025 itaendelea kukumbukwa kama siku ya uthibitisho wa dhamira ya
kweli ya Serikali ya Mapinduzi ya Kisekta.
Ni siku ambayo Rais
wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan,
alisimama mbele ya wakulima, watafiti, wanasayansi na wadau wa kilimo katika
viwanja vya Nane Nane Nzuguni, Dodoma na kutoa kauli ya matumaini.
Alitangaza mustakabali mpya wa kilimo cha umwagiliaji kama
mustakabali unaojengwa juu ya sayansi, teknolojia na bioteknolojia ya kilimo
ili kulinda uhakika wa chakula na kuongeza thamani ya mazao.
Rais Samia alisema kwa msisitizo: “Natamani kuona Tume ya
Taifa ya Umwagiliaji ikiendelea kufanya kazi, kuchochea uzalishaji, na
kuhakikisha huduma hizi zinamfikia mkulima wa kila ngazi — mdogo, wa kati, na
mkubwa.”
Kauli hii haikuwa tu mwito wa kisera, bali ni tangazo la
mapinduzi ya uzalishaji wa chakula, yanayounganisha teknolojia ya umwagiliaji
na bioteknolojia ya kisasa katika kuzalisha mbegu bora, kustahimili mabadiliko
ya tabianchi, na kuleta tija.
Serikali imewekeza kwa kiwango kikubwa katika sekta ya
umwagiliaji ili kukabiliana na changamoto za mabadiliko ya tabianchi.
Katika mwaka wa fedha 2024/2025 pekee, zaidi ya hekta
700,000 zimewekewa miundombinu ya umwagiliaji na kuanza kutumika.
Hatua hizi ni pamoja na ujenzi wa skimu mpya 63 na ukarabati
wa skimu 48, ujenzi wa mabwawa 114 na miundombinu katika mabonde 22 ya
kimkakati, sambamba na uanzishaji wa mashamba makubwa ya pamoja sita.
Aidha, imefanya upembuzi yakinifu na usanifu wa miradi 527
ambayo inaendelea mpaka sasa.
Na baada ya miradi hiyo kukamilika, eneo la umwagiliaji
litaongezeka kutoka hekta 727,000 za sasa hadi hekta 1.2 milioni.
Kwa muktadha huo, hiyo ni hatua ambayo si tu inapunguza
utegemezi wa mvua, bali pia inaleta fursa ya kupanua matumizi ya mbegu bora za
kibioteknolojia zinazohitaji usimamizi sahihi wa maji ili kutoa mavuno ya juu.
Maonesho ya Nane Nane mwaka huu yalionesha sura mpya ya
Tanzania katika teknolojia ya kilimo.
Kuanzia mifereji ya kisasa, mifumo ya kunyunyizia maji
(sprinklers), umwagiliaji wa matone (drip irrigation), hadi mitambo mikubwa ya
centre pivot — yote yalitoa taswira ya taifa linalokimbizana na wakati.
Lakini kilichobeba uzito zaidi ni ujumuishaji wa teknolojia
hizi na bioteknolojia.Matumizi ya mbegu zinazostahimili ukame, mbegu zinazokua
kwa muda mfupi, na mazao yanayoboreshwa kimaumbile ili kuongeza virutubisho.
Waziri wa Kilimo, Hussein Bashe, alibainisha kuwa mashamba
ya mbegu ya serikali yenye zaidi ya hekta 13,000 tayari yanatumia mifumo ya
umwagiliaji pamoja na mbegu za kisasa zinazozalishwa na Taasisi ya Utafiti wa
Kilimo Tanzania (TARI).
Benedict Kahemele wa Ilula mkoani Iringa ni mfano wa
mabadiliko haya. alianza kulima nyanya na mahindi kwa mvua, alikumbwa na hasara
mara kwa mara. Lakini tangu aanze kutumia skimu ya umwagiliaji na mbegu bora
kutoka TARI na matumizi ya teknolojia za bioteknolojia, hali imebadilika.
“Sasa nalima misimu yote bila hofu ya ukame, nyanya zangu
zinavumilia magonjwa, na kipato changu kimenipatia nyumba yangu na wapangaji
wangu,” anasema Kahemele huku akionesha kufurahia kilimo.
Hadithi yake ni kielelezo cha jinsi sayansi na bioteknolojia
zinavyobadilisha maisha ya kila siku ya Watanzania kupitia kilimo chenye tija.
Tume ya Taifa ya Umwagiliaji, chini ya uongozi wa Raymond
Mndolwa, imekuwa kiungo cha kufanikisha mabadiliko haya.
Kupitia ufadhili wa serikali, tume imenunua pampu 2,000,
mitambo ya kuchimba visima, na vifaa vya kusambazwa nchi nzima.
Aidha, Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB)
imeongeza mtaji wake kutoka shilingi bilioni 60 hadi bilioni 442, na kutoa
mikopo ya pembejeo, ikiwemo zile za bioteknolojia kama mbegu bora na viuatilifu
salama kwa mazingira.
Katika kilele cha hafla hiyo, Rais Samia alizindua Maabara
ya Rufaa ya Taifa ya Kilimo jijini Dodoma. Maabara hii, chini ya TARI, ni
injini ya mapinduzi ya 'agricultural biotechnology' nchini kwa utambuzi wa
magonjwa ya mimea na visumbufu.
Pia kazi nyingine ya maabara hiyo ni mahsusi kwa uchunguzi
wa afya ya udongo, ubora wa mbegu, utafiti wa viini lishe ili kuboresha thamani
ya mazao na udhibiti wa sumukuvu (aflatoxin).
Kwa maabara hiyo, sera na maamuzi ya kilimo yatajengwa juu
ya ushahidi wa kisayansi.
Hii inamaanisha Tanzania sasa inaweza kuzalisha mbegu
zilizoboreshwa kitaalamu (improved seeds), kustahimili ukame, magonjwa na hata
kuongeza mazao yenye lishe bora kwa afya ya jamii.
Ongezeko la eneo la umwagiliaji na uwekezaji katika bioteknolojia
linaashiria:
Kuongezeka kwa uzalishaji wa mazao kwa zaidi ya asilimia 50
katika miradi ya umwagiliaji.
Ajira mpya zaidi ya laki mbili vijijini kupitia kilimo na
mnyororo wa thamani.
Mapato ya wakulima kuongezeka maradufu kutokana na mbegu bora
na mavuno thabiti.
Hii siyo tu takwimu, bali ni uhakika wa heshima, kipato, na
maisha bora kwa jamii ya wakulima vijijini.
Kwa hatua hizi, Tanzania sasa inajipanga sambamba na mataifa
yanayotumia bioteknolojia ya kilimo kama India, Brazil na Afrika Kusini.
Uwekezaji wa umwagiliaji unaounganishwa na mbegu bora za
kisayansi unaipa Tanzania nafasi ya kuwa ghala la chakula la Afrika Mashariki
na mshindani katika soko la kimataifa.
Rais Samia amesisitiza kuwa ifikapo mwaka 2030, sekta ya
kilimo lazima iwe imara, shindani, na yenye kipato cha uhakika.
Pia alisisitiza Dira ya Taifa 2025-2050 pia imezingatia kwa
uzito masuala haya ikiwemo uzalishaji wa chakula wa kutosheleza taifa na ziada
ya kuuza nje.
Pia mauzo ya mazao yenye thamani kubwa na bora kiafya (biofortified
crops),
ajira endelevu kwa vijana na wanawake vijijini na uchumi wa
kilimo unaotegemea sayansi na ubunifu.
Mapinduzi haya si jukumu la serikali pekee. Ni mwaliko kwa
kila mdau — kutoka mtafiti wa maabara, mzalishaji wa mbegu, mhandisi wa
umwagiliaji, taasisi za fedha, hadi mlaji wa mwisho.
Kama alivyoeleza Rais Samia: “Mnyororo wote wa kilimo lazima
ukae vizuri.” Ni wakati wa kuhakikisha kila kiungo kinang’aa — kwa msaada wa
umwagiliaji wa kisasa na bioteknolojia ya kilimo — ili Tanzania ifikie uhuru wa
chakula na ustawi wa Taifa zima.
Na katika kufanikisha hilo, Tume ya Taifa ya Sayansi na
Teknolojia (COSTECH) ni ya msingi kwa mtazamo wa kisera na kiutekelezaji, ndio
kiungo kikuu cha kuratibu tafiti zote za bioteknolojia ya kilimo nchini.
Pia COSTECH ni injini
ya kisayansi nyuma ya maono ya Rais Samia kuhusu kilimo cha kisasa –
ikihakikisha kuwa uwekezaji wa umwagiliaji, mbegu bora na utafiti wa kisayansi
vinaunganishwa katika mnyororo wa thamani wa kilimo Tanzania.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan akikata utepe kuashiria uzinduzi wa Maabara ya Rufaa ya Taifa ya Kilimo Agosti 8, 2025 iliyopo Mtumba Jijini Dodoma.
Baadhi ya wataalamu wa
Taasisi ya Utafiti wa Kilimo Tanzania (TARI) wakifurahia moja ya kazi za usindikaji
zinazofanywa na taasisi hiyo kwa kunyanyua chupa yenye mvinyo uliotengenezwa kwa
'Bibo la Korosho' , kwenye maonesho ya nanenane kitaifa mwaka 2020 yaliyofanyika eneo la Nyakabindi, Bariadi mkoani Simiyu.






No comments