Header Ads

DKT. ANDREW KOMBA, AFISA MTENDAJI MKUU NFRA ANAYEIMARISHA UHIFADHI WA CHAKULA NCHINI

Waziri wa Kilimo, Mhe. Hussein Bashe akikagua maghala ya Wakala wa Taifa wa Hifadhi ya Chakula (NFRA) yaliyopo eneo la Mazwi, Sumbawanga mjini, mkoani Rukwa,Julai 16, 2024. Kushoto ni   Afisa Mtendaji Mkuu (CEO) wa Wakala wa Taifa Hifadhi ya Chakula (NFRA), Dkt. Andrew Komba.

...........................................

Imeandaliwa na Dotto Mwaibale

(0754-362990)

CHAKULA ni muhimu sana kwa kiumbe chochote chenye uhai hivyo kinapokosekana kinasababisha vifo na kudorora kwa uchumi kutokana na waathirika wa njaa kushindwa kufanya shughuli za uzalishaji mali.

Kuna mifano michache ambayo tunaweza kuiona kutoka nchi mbalimbali ambazo ziliwahi kukumbwa na baa la njaa kutokana na ukame, vita, mafuriko zikiwemo nchi za Somalia na Sudani ambapo waathirika wakubwa walikuwa ni wanawake na watoto.

Katika nchi yetu tuliwahi kupatwa na changamoto ya ukosefu wa chakula baada ya kuibuka ukame katika baadhi ya mikoa na kutokana na upungufu huo wa chakula Serikali ilianzisha Wakala wa Taifa wa Hifadhi ya Chakula (NFRA) na hiyo ilikuwa kwenye miaka ya 1973 na 1975 ambapo tulilazimika kununua mahindi ya njano kutoka Marekani kwa ajili ya kukabiliana na njaa.

Kipindi hicho nchi ilipata athari kubwa ya upungufu wa chakula hivyo kushindwa kumudu mahitaji ya ndani na kufikia hatua ya kuagiza kutoka nje ya nchi.

Mwaka 1976 Serikali ilianzisha chombo kilichoitwa Hifadhi ya Taifa ya Chakula (SGR) kwa ajili ya kupunguza joto la uhaba wa chakula ambapo chombo hicho baadae kwa nyakati tofauti kilifanyiwa mabadiliko na kuwa NFRA kikiwa chini ya Wizara ya Kilimo.

Dira ya NFRA ni Kuwa Wakala wa kuaminika wenye uwezo wa kukabiliana na upungufu wa chakula kwa wakati na dhima yake ni Kuhakikisha upatikanaji wa akiba ya chakula cha kimkakati wakati wa upungufu wa chakula kwa kununua, kuhifadhi, kuzungusha na kutafuta masoko ya chakula kwa ufanisi na kwa manufaa ya jamii.

Kuanzia hapo NFRA kupitia maafisa wake watendaji wa kuu waliowahi kuhudumu kwenye nafasi hiyo na wasaidizi wao wamekuwa na mikakati mbalimbali ya kuhakikisha nchini inakuwa na hifadhi ya kutosha ya chakula.

Dkt. Andrew Komba ni Afisa Mtendaji Mkuu (CEO) wa Wakala wa Taifa Hifadhi ya Chakula (NFRA) ambaye leo nitaelezea kwa ufupi anavyopambana kuhakikisha NFRA inaendelea kujiimarisha kwa kuwa na mipango endelevu ya uhifadhi wa chakula nchini kwa kushirikiana na watendaji wenzake na Serikali chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan akisaidiwa na Waziri wa Kilimo, Hussein Bashe.

Katika kipindi hiki tumeona ujenzi wa maghala mengi ya kisasa ya kuhifadhi chakula yakijengwa jambo ambalo linaonesha  NFRA kupitia Serikali walivyojidhatiti kuhakikisha nchi inakuwa na hifadhi kubwa ya chakula ambapo imefungua vituo vya ununuzi wa nafaka kwa wakulima katika kanda zake zote nchini..

Mbali ya kujenga maghala ya kisasa na vihenge vya kuhifadhi chakula katika kanda saba za NFRA pia Afisa Mtendaji Mkuu wa NFRA, Dkt. Andrew Komba amekuwa akikutana na wadau mbalimbali kutoka ndani na nje ya nchi kwa ajili ya kubadilishana uzoefu wa namna bora ya kuhifadhi chakula ili nchi iwe chakula cha kutosha na ziada kuuzwa nje ya nchi pasipo kuathiri hifadhi hiyo ya chakula.

NFRA imekuwa ikipaa kwa mafanikio chini ya uongozi wa Dkt. Andrew Komba kutokana na kujipanga vizuri na timu yake huku wakizingatia Maadili, Ufanisi wa kazi. Kuaminika, Uweledi, Uadilifu, kumjali mteja, Uwazi, Uwajibikaji, Ubunifu na kufanya kazi kwa pamoja.

Mbali ya kufanya kazi kwa ufanisi na uweledi wafanyakazi wa NFRA wamejikiti zaidi kwenye majukumu yao ya Kuhifadhi akiba ya chakula toshelevu kwa mahitaji ya nchi, Kununua, kuhifadhi na kutoa akiba ya chakula ili kukabiliana na majanga, Kuzungusha na kutafuta masoko ya chakula ili kupunguza mfumuko wa bei na kuingiza mapato na kutoa huduma mbalimbali za uhifadhi ili kuongeza mapato.

Katika mashirikiano na wadau wengine wa ndani na nje kwa ajili ya kuuza ziada ya mahindi Wizara ya Kilimo ilisaini makubaliano ya kuuza tani 500,000 za Mahindi Jamhuri ya Demokrasia ya Congo.

Makubaliano hayo yalifanyika baina ya NFRA na Wajumbe wa Jimbo la Katanga, walioongozwa na Gavana wa Jimbo la Katanga, Jacques Kyabula Katwe ambapo utiaji Saini wa mkataba huo ulifanyika kati ya Afisa Mtendaji Mkuu wa NFRA Dkt. Andrew Komba pamoja na Mkurugenzi wa Kampuni ya Quincy, Yuma Jesse ukishuhudiwa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo. Gerald Mweli.

Baada ya kusaini mkataba huo walijadiliana na Gavana huyo na kukubaliana juu ya mahusiano ya muda mrefu ambapo mkataba huo una awamu mbili za mauziano ya mahindi ambapo kwa awamu ya kwanza nchi ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo itakabidhiwa tani 200,000 za mahindi meupe huku tani 300,000 za mahindi hayo zikitarajiwa kukabidhiwa katika awamu ya pili.

Afisa Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Taifa Hifadhi ya Chakula (NFRA) Dkt. Andrew Komba katika kuimarisha mahusiano na makundi mengine ya watu alipata fursa ya kukutana na wafanyabiashara wa Nafaka kutoka Falme za kiarabu (EAU) walipotembelea Banda la Wakala katika maonesho ya Wakulima Nane Nane jijini Dodoma na kujadili namna gani wanaweza pata fursa ya mashirikiano ya biashara ya Nafaka na NFRA.

Aidha NFRA na Wizara ya Kilimo, Umwagiliaji, Maliasili na Mifugo ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (WKUMM) zilifikia makubaliano ya kuwa na ushirikiano kwenye masuala ya ununuzi/mauzo ya nafaka, uhifadhi wa akiba ya chakula, kubadilishana uzoefu na kujengeana uwezo katika masuala ya uendeshaji wa hifadhi ya chakula. Makubaliano yaliyofanyika Desemba 21, 2023 ambapo Katibu Mkuu wa WKUMM  Seif Shabani Mwinyi na Afisa Mtendaji Mkuu wa NFRA Dkt. Andrew Komba walisaini Randama itayoongoza utekelezaji wa makubaliano hayo.

Dkt. Komba kwa leo nikomee hapa endelea kufanya kazi hiyo  kubwa ya uhifadhi wa chakula kwa ajili ya Taifa la Tanzania huku mkijua kuwa chakula ndio kila kitu katika maisha ya wanadamu. Kazi Iendelee.

Ujumbe kutoka Wizara ya Kilimo Umwagiliaji Maliasili na Mifugo ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar walipofanya ziara ya kutembelea Wakala wa Taifa wa Hifadhi ya Chakula (NFRA). Ujumbe huo uliwajumuisha Maafisa wa tatu akiwemo Zainabu Moyo, Ally Basha na Mhandisi Salmin Hassan Ally.
Dkt. Komba katika kuimarisha mahusiano na makundi mengine ya watu alipata fursa ya kukutana na wafanyabiashara wa Nafaka kutoka Falme za kiarabu (EAU) walipotembelea Banda la Wakala katika maonesho ya Wakulima Nane Nane jijini Dodoma na kujadili namna gani wanaweza pata fursa ya mashirikiano ya biashara ya Nafaka na NFRA.

Wajumbe wa Jimbo la Katanga, walioongozwa na Gavana wa Jimbo la Katanga, Jacques Kyabula Katwe ambapo utiaji Saini wa mkataba huo ulifanyika kati ya Afisa Mtendaji Mkuu wa NFRA Dkt. Andrew Komba pamoja na Mkurugenzi wa Kampuni ya Quincy, Yuma Jesse ukishuhudiwa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo. Gerald Mweli wakionesha mkataba wa makubaliano hayo. 

Naibu Waziri wa Kilimo Mhe. David Silinde(Mb), akimkabidhi Mkurugenzi wa Huduma Saidizi wa NFRA, Bw. Mohamedi Ally, cheti cha umiliki wa Maghala ya Mradi wa kudhibiti sumu kuvu nchini TANPACK na kuwa mmiliki halali wa Maghala hayo, makabidhiano hayo yamefanyika tarehe 12 Desemba, 2023 katika kata ya Mrijo Kijiji cha Mrijo Chini Wilayani Chemba. Maafisa wa Wakala wa Taifa wa Hifadhi ya Chakula (NFRA) na Wizara ya Kilimo, Umwagiliaji, Maliasili na Mifugo ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (WKUMM) wakisaini makubaliano ya kuwa na ushirikiano kwenye masuala ya ununuzi/mauzo ya nafaka, uhifadhi wa akiba ya chakula, kubadilishana uzoefu na kujengeana uwezo katika masuala ya uendeshaji wa hifadhi ya chakula. 

No comments

Powered by Blogger.