Header Ads

SAIMON SIRILO KUZINDUA KITABU CHA UJASIRIAMALI ITIGI, SINGIDA


 Na Dotto Mwaibale, Singida

JINA la Saimon Sirilo kwa wadau wa ujasiriamali wa Mkoa wa Singida na ya jirani siyo geni kutokana na jinsi anavyojitoa kwa hali na mali kufundisha makundi ya watu katika kufanya shughuli mbalimbali za ujasiriamali ili kujikomboa kiuchumi.

Sirilo ni mkufunzi mbobezi wa masuala ya ujasiriamali ambaye makao makuu yake yapo Itigi mkoani Singida.

Ni watu wachache mno wenye moyo wa kujitolea kama alionao Sirilo wakati wote amekuwa ni mwalimu wa kutoa elimu hiyo tena kwa gharama zake akishirikiana na wadau wengine wa maendeleo.

Licha ya kujitolea kwa kiasi hicho ameona haitoshi hivyo ameandika kitabu maalumu kinachoelezea masuala mbalimbali ya ujasiriamali lengo likiwa ni kuwasaidia wajasiriamali wakongwe na chipukizi kujifunza mbinu za ujasiriamali.

Kitabu hicho anatarajia kukizindua rasmi Disemba 13, 2025.

Akizungumza na waandishi wa habari Sirilo alisema watu wengi wamekuwa na shauku ya kujua ndani ya kitabu hicho alichokipa jina la “MJASIRIAMALI WA LEO, TAJIRI WA KESHO” kutakuwa na mambo gani.

Sirilo alisema ndani ya kitabu hicho kuna mambo mengi ya msingi yanayohusu masuala ya ujasiriamali na mbinu za kutengeneza pesa kupitia kazi hiyo ambayo haimbagui mtu kwa umri wake.

“ Napenda kuwajulisha wadau wangu kuwa mada zote ambazo huwa nawafundisha wajasiriamali, sasa nimeziweka katika maandishi ili yaendelee kuwa msaada wakati wote hata kama sitakuwepo,” alisema Sirilo.

Sirilo aliyataja masomo yaliyopo katika kitabu hicho kuwa ni Fursa adhimu zilizopo mkoani Singida, Ufugaji wa Kuku, Kilimo cha Matikiti, Bajeti, Mauzo na Masoko, Huduma kwa wateja na Elimu ya fedha.

Alitaja masomo mengine kuwa ni baadhi ya Biashara zinazoweza kumtoa mtu haraka kiuchumi na bidhaa za viwanda vidogo ikiwemo, Sabuni aina zote, karanga za mayai, klipsi, batiki, keki na kadhalika.

Aidha, Sirilo alisema Kitabu hicho kitakuwa ni mkombozi kwa wajasiriamali, hivyo alitumia nafasi hiyo kuwaomba wananchi wote pamoja na wajasiriamali kufika kushiriki kwenye uzinduzi huo ili waweze kujipatia nakala ya kitabu hicho kwa bei ya Sh.10000 tu.

Alisema uzinduzi huo utafanyika kuanzia saa 6:00 mchanna Ukumbi wa Penda- Meri uliopo Mjini Itigi.

Kwa mawasiliano zaidi kuhusu uzinduzi huo unaweza kuwasiliana na Saimon Sirilo Mwandishi wa kitabu kwa namba ya simu 0744445060.

No comments

Powered by Blogger.