Header Ads

COSTECH INAVYO SAIDIA WABUNIFU NCHINI

Dk. Cecilia China ambaye ni mwanasayansi mahiri Mwanamke na Mhadhiri kutoka Taasisi ya Afrika ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela na Mwanzilishi wa Kampuni ya Afritech Organe Leather Co.Ltd, akizungumza na waandishi wa habari (hawapo pichani) katika Maonesho ya Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu yanayoendelea kwenye viwanja vya Usagara Jijini Tanga Agosti 19, 2026.
..................................

Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH),  imekuwa na mchango mkubwa wa kuwawezesha wabunifu mbalimbali nchini kusonga mbele.

COSTECH imekuwa ikitoa ushauri na Rasilimali fedha kwa wabunifu mbalimbali.

Miongoni mwa wabunifu hao ni Dk. Cecilia Rolence China ambaye ni mwanasayansi mahiri Mwanamke na Mhadhiri.

China amepata umaarufu mkubwa kitaifa na kimataifa kutokana na ugunduzi wake wa kimapinduzi wa kutumia maganda ya korosho na kutengeneza dawa asili na rafiki wa mazingira ambayo inatumika kutengeneza ngozi.

Dk.China akizungumza kwenye Maonesho ya Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu yanayoendelea kwenye viwanja vya Usagara Jijini Tanga amesema kuna wadau mbalimbali wa kimataifa na kitaifa waliomwezesha kufikia hatua hiyo yenye mafanikio makubwa.

Ameyataja baadhi ya mafanikio hayo kuwa ni kuanzisha Kampuni ya AfriTech Organic Leather.

Alisema kampuni hiyo inazalisha ngozi ghafi zilizosindikwa kwa maganda ya korosho na kutengeneza bidhaa za ziada kama mikoba ya kike, pochi, na vifaa vya ofisini vyenye ubora wa kimataifa.

 “ Kampuni yangu ya kipekee ya kiteknolojia ya kuchakata takataka za korosho na kuzigeuza kuwa kemikali salama ya ngozi imesajiliwa kisheria na kupata hataza ya kiugunduzi na kunipa umiliki wa teknolojia duniani,” alisema China.

Alisema kupitia taasisi yake, amefanikiwa kutoa mafunzo ya vitendo (Capacity Building) kwa zaidi ya wanawake na vijana 300.

Mafanikio mengine yaliyopatikana ni kujifunza mnyororo mzima wa thamani wa ngozi (kuanzia usindikaji wa asili hadi ushonaji wa bidhaa.

Aliongeza kuwa COSTECH kupitia mfuko wa Serikali wa kusaidia wabunifu  imekuwa ikitoa ruzuku ndogo ndogo  na gharama za kuwezesha ushiriki wake kwenye maonesho ya kitaifa ya ugunduzi, jambo lililomsaidia kupata mtaji wa awali wa majaribio ya kijamii.

Alitaja baadhi ya taasisi na wadau wengine waliomsaidia rasilimali fedha ulitokana na  ruzuku za kiutafiti na ufadhili wa masomo ya juu kutoka mashirika makubwa ya kimataifa na kikanda.chini ya UNESCO.

Alisema UNESCO  ndiyo taasisi iliyompa msukumo mkubwa zaidi wa kifedha ambapo iliweza kumtunuku ruzuku ya Tuzo ya Fellowship ya takriban USD 50,000 (zaidi ya Shilingi Milioni 130 za Kitanzania).

“Fedha hizi zilitumika kununulia vifaa vya kisasa vya kimaabara, kemikali za majaribio, na kuajiri wasaidizi wa utafiti ili kuongeza kasi ya uzalishaji wa dawa hiyo ya maganda ya korosho.

Taasisi nyingine ni Benki ya Maendeleo ya Afrika, ambayo ilifadhili masomo yake ya ngazi ya juu ya Uzamivu (PhD).

Aliongeza kuwa  ufadhili huo uliondoa vikwazo vya kifedha na kumruhusu kujikita kikamilifu katika utafiti uliomfikisha kwenye ugunduzi huo wa kipekee.

Mkurugenzi Mkuu wa COSTECH, Dk. Amos Nungu, akizungumza kwenye Maonesho ya Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu yanayofanyika katika viwanja hivyo jijini humo akieleza maendeleo ya tafiti na bunifu zinazofanyika nchini alisema Tanzania ina ubunifu wa aina mbalimbali, ikiwemo unaolenga kuongeza thamani katika mazao ya kilimo, mifugo na maeneo mengine mbalimbali. 

“Kwa upande wa tafiti tuko vizuri kama nchi, tunatoa nafasi ya kuboresha,” alisema Dk. Nungu.

Alisema kuwa,baadhi ya wabunifu wamekuwa wakifanya mambo yenye kuleta athari chanya katika jamii kupitia tafiti na bunifu zao.

Mbunifu mwingine aliyewezeshwa na COSTECH Lusano Luvanda ambaye ni mwanafunzi  kutoka Chuo Kikuu cha Sayansi na Teknolojia Mbeya (MUST), na Mkurugenzi Mtendaji (CEO) wa kampuni au maabara ya ubunifu ya Ecoflame Labs na Beyond Horizon, inayojihusisha na masuala ya teknolojia na ujasiriamali wa vijana  mbunifu wa kifaa kinachoitwa Atlas kinachotengeneza nishati gas ya kupikia  kutoka kwenye maji akizungumzia ubunifu wake.

Alisema alisukumwa na dhamira ya kutengeneza nishati ya umeme kwa ajili ya matumizi ya nyumbani.

Aidha, Luvanda alisema baada ya ubunifu huo alisaidiwa na Chuo Kikuu cha Sayansi na Te
knojia cha Mbeya (MUST) ambapo amewaomba wawekezaji kusaidia ubunifu huo ili kuifanya nchi yetu kuacha matumizi ya kutumia nishati kama petroli kutoka nje ambayo inapatikana kwa gharama kubwa na kuchangia uharibifu wa mazingira.

“Naishukuru COSTECH kwa kuniwezeha kufikia hatua kubwa ya ubunifu wangu kwa kunipa fedha tangu nilipoanza ubunifuu ambao umeonesha tija,” alisema Luvanda.

Wabunifu wengine ambao wameishukuru COSTECH ni Maganga Mabula ambaye amebuni mfumo unaoitwa Mnyama Check App na Heleni Janja.  

Mfumo huo unasaidia wakulima kujua afya za wanyama wanaofuga na mahali walipo.

Mbunifu mwingine kutoka COSTECH, Ibrahim Meshack ambaye amebuni mashine ya kukokotwa ijulikayo kama Smart Shamba Planter mahususi kwa upandaji wa mbegu  mbalimbali kama, mahindi, mpunga. Dengu, karanga na mazao mbalimbali.

 Meshack alitaja sifa ya Planter hiyo ni kupanda kwa muda mfupi na kwa gharama nafuu na inaweza kuvutwa kwa guta, Power Tiller na trekta.

“Planter hii inakwenda kuongeza wingi wa mazao shambani na kipato,” alisema Meshack.


Dk. Cecilia China akionesha vifungashio vyenye kemikali zilizotengenezwa na kampuni yake kwa ajili ya kutengeneza ngozi.


Mbunifu Maganga Mabula akizungumzia mafanikio ya ubunifu wake. Kulia ni Mkurugenzi Mkuu wa COSTECH, Dk. Amos Nungu.

Mbunifu kutoka Tume ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH), Ibrahimu Meshack akitoa maelezo ya Planter aliyoibuni kwa ajili ya kupanda mbegu mbalinbali.

Mbunifu Dk. Cecilia China akiwajibika kwenye Maonesho hayo
Bidhaa za ngozi zinazotengenezwa na Kampuni ya AfriTech Organic Leather inayo milikiwa na Dk. Cecilia China.

Kemikali za kutengeneza ngozi zinazotengenezwa na Kampuni ya AfriTech Organic Leather inayo milikiwa na Dk. Cecilia China.


Habari hii imeandaliwa na Dotto Mwaibale namba ya simu 0754362980

No comments

Powered by Blogger.