DK. MPANGO AIPONGEZA TARI KWA JARIBIO LA KWANZA LA ZAO LA VIAZI MVIRINGO
Makamu wa Rais Mstaafu Dk. Philip Mpango, (wa tatu kusho) akiwa na Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Utafiti wa Kilimo (TARI), Thomas Bwana (wa pili kulia) wakionesha viazi mviringo ambavyo vimetokana na jaribio la kwanza la mbegu ya viazi mviringo lililofanywa na TARI na kuonesha mafanikio makubwa katika shamba la Dk. Mpango ililopo Kijiji cha Mayamaya, Wilaya ya Bahi mkoani Dodoma. Kutoka kushoto ni Mkurugenzi Uhaulisha wa Teknolojia TARI, Dk. Sophia Kashenge, Mtafiti wa mbegu hiyo, Dk.Owekisha Kwegizela na Afisa Mawasiliano Mkuu TARI, Eveline Mpasha.
.....................
Na Mwandishi
Wetu, Dodoma
Makamu wa
Rais Mstaafu Dk. Philip Mpango, ameipongeza
Taasisi ya Utafiti wa Kilimo (TARI) kwa kusimamia jaribio la kwanza la Mbegu ya
viazi mviringo ambalo limeonesha mafanikio makubwa katika shamba lake lililopo
Kijiji cha Mayamaya, Wilaya ya Bahi mkoani Dodoma.
Kutokana na
mafanikio hayo Dk. Mpango amewataka wakazi wa Mkoa wa Dodoma kuchangamkia fursa
ya kulima zao hilo pindi utafiti utakapokamilika.
“ Wakazi wa Dodoma sasa tuanze kuchangamkia hii fursa na TARI wako tayari kutusaidia kwa kutupatia mbegu bora zinazofaa zaidi na hii itatusaidia kuwa na chakula na kipato kwa ajili ya kusaidia watoto wetu kwenda shule. Dodoma siyo nusu jangwa, ni maarifa tu ya kupata na kuvuna maji kwa ajili ya kuendeleza kilimo, hatuwezi kuendelea kwa kutegemea mtama, mahindi, zabibu au alizeti pekee lazima tuongeze na mazao mengine” alisema Dk. Mpango.
Jaribio hilo
la kwanza lilichukua siku 104 za
majaribio shambani hadi kuvuna limedhihirisha kuwa zao la viazi mviringo
linaweza kustawi katika mazingira ya
Mkoa wa Dodoma na kuufanya kuwa na fursa mpya ya zao la chakula na
biashara ambalo linaweza kuwasaidia wananchi wa mkoa huo kuondokana na
umasikini.
Akiongelea kuhusu jaribio hilo na matokeo yake, Mkurugenzi Mkuu wa TARI, Dk. Thomas Bwana
amemshukuru Dk. Mpango kwa kukubali TARI kuweka jaribio la viazi mviringo katika shamba lake na kueleza kuwa TARI imepanga kuweka majaribio ya zao hilo
kwa wakulima wadogo wanaolima kwa kutegemea mvua.
Katika hatua
nyingine Dk. Bwana ameongeza kuwa TARI
itaendelea na majaribio ya utafiti wa mazao katika maeneo mbalimbali
nchini ili kuondoa dhana iliyojengeka
ya ikolojia hii ni ya mazao fulani pekee na kuwaomba
wananchi hususani wakulima kuwakaribisha
TARI kuweka majaribio ya utafiti katika mashamba yao.
Kwa mujibu
wa Mtafiti Kiongozi wa zao la viazi
mviringo kutoka kituo cha TARI - Uyole Dk. Owekisha Kwigizila, mbegu hiyo mpya ya TARI ina sifa ya kukomaa kwa muda
mfupi wa takribani siku 90, kustahimili ukame na baadhi ya magonjwa pamoja na
kuwa na uwezo wa kuzalisha tani 35 hadi 40 kwa hekta moja.
Baadhi ya
wakazi wa Kijiji cha Mayamaya walioshiriki katika zoezi la uvunaji wa viazi
hivyo wameonesha kustaajabishwa na kustawi kwa zao hilo katika Kijiji hicho cha
Mayamaya na kueleza kuwa hiyo ni mara yao ya kwanza kuona zao hilo la viazi
likilimwa na kustawi Mkoani Dodoma na
kuonyesha shauku kubwa ya kujaribu kulima zao hilo katika mashamba yao,
Utafiti huo
wa zao la viazi Mkoani Dodoma bado unaendelea ili kukamilisha hatua zote muhimu
kabla ya mbegu hiyo kuingizwa rasmi sokoni.
Mafanikio
hayo yanaendelea kuthibitisha kuwa Dodoma inaweza kuzalisha mazao mbalimbali ya
chakula na biashara kupitia nguvu ya utafiti, ubunifu na teknolojia za
kilimo na kubadilisha maisha ya wakulima
wa Mkoa wa Dodoma.
Makamu wa Rais Mstaafu Dk. Philip Mpango na Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Utafiti wa Kilimo (TARI), Thomas Bwana wakionesha viazi mviringo ambavyo vimetokana na jaribio la kwanza la mbegu ya viazi mviringo lililofanywa na TARI na kuonesha mafanikio makubwa katika shamba lake lililopo Kijiji cha Mayamaya, Wilaya ya Bahi mkoani Dodoma.



No comments