Header Ads

MTAFITI DK. CECILIA CHINA; KUTOKA SHILINGI MILIONI 20 HADI SAFARI YA UCHUMI WA DOLA TRILIONI MOJA

Mtafiti Dk. Cecilia China ambaye ni mwanasayansi na Mhadhiri kutoka Taasisi ya Afrika ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela (NM-AIST) na Mwanzilishi wa Kampuni ya Afritech Organe Leather Co.Ltd, akizungumza na waandishi wa habari (hawapo pichani) Agosti 19, 2026 katika Maonesho ya Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu Jijini Tanga kuhusu mafanikio makubwa baada ya kugundua maganda ya korosho kuzalisha kimiminika kinachojulikana kama Cashew Nut Shell Liquid (CNSL), ambacho hutumika kutengeneza dawa inayotumika katika usindikaji wa ngozi. 

.........................

SERIKALI ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania mwaka 1986 ilichukua hatua muhimu ya kuimarisha uratibu, ukuzaji na usimamizi wa tafiti za kisayansi na teknolojia kwa kuanzisha Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH) kupitia Sheria ya Bunge Na. 7 ya mwaka huo.

Taasisi hiyo ilirithi majukumu ya lililokuwa Baraza la Taifa la Utafiti wa Kisayansi (UTAFITI) na kupewa jukumu la kuwa mshauri mkuu wa Serikali katika masuala ya sayansi, teknolojia na matumizi ya matokeo ya tafiti katika kukuza maendeleo na uchumi wa taifa.

Tangu kuanzishwa kwake, COSTECH imekuwa kichocheo muhimu cha tafiti na ubunifu, ambapo baadhi ya bunifu zimeingia katika uzalishaji na biashara, zikionyesha namna uwekezaji katika sayansi na teknolojia unavyoweza kufungua fursa za ajira, viwanda na biashara ya kimataifa.

Mtafiti Dk. Cecilia China na Afisa Masoko wa Kampuni hiyo, Emile Gabriel Isangya (kulia), wakionesha bidhaa za ngozi zinazotengenezwa na kiwanda chao.

..................................

Miongoni mwa mifano hiyo ni wa Dk. Cecilia Rolence China, mtafiti kutoka Taasisi ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela (NM-AIST), mama wa watoto wawili, mjasiriamali na mmiliki wa kampuni ya Kampuni ya AfriTech Organic Leather pamoja na kiwanda kilichopo jijini Arusha.

Mwaka 2019, Dk. Cecilia alikuwa miongoni mwa washindi wa Mashindano ya Ubunifu ya MAKISATU na kupitia ushindi huo alipata ufadhili wa Shilingi milioni 20 kutoka Serikali kupitia COSTECH. Uwekezaji huo wa awali katika wazo la ubunifu leo umefikia hatua ya uzalishaji na biashara.

Dk. Cecilia analenga kutumia maganda ya korosho kuzalisha kimiminika kinachojulikana kama Cashew Nut Shell Liquid (CNSL), ambacho hutumika kutengeneza dawa inayotumika katika usindikaji wa ngozi.

Ubunifu huo unaunganisha sekta mbili muhimu za uchumi wa Tanzania—korosho na mifugo—katika mnyororo mmoja wa thamani.

Mtafiti Dk. Cecilia China, akionesha vipande vya ngozi ambayo imekwisha andaliwa na kiwanda hicho tayari kuwa sokoni na kutengeneza bidhaa mbalimbali.

.................................

Tanzania ilizalisha zaidi ya tani 528,000 za korosho katika msimu wa 2024/25, huku maganda yakifikia wastani wa asilimia 70 hadi 75 ya uzito wa korosho mbichi. Hii inaonesha ukubwa wa malighafi inayoweza kupatikana iwapo korosho zitachakatwa ndani ya nchi.

Kwa upande mwingine, Tanzania ilikuwa na zaidi ya ng’ombe milioni 39.2 mwaka 2024, mbuzi milioni 28.6 na kondoo milioni 9.7, huku uzalishaji wa ngozi ghafi ukifikia tani 55,410.

Takwimu hizi zinaonesha kuwa Tanzania tayari ina malighafi za kutosha, lakini changamoto imekuwa ni kuongeza thamani kabla ya malighafi hizo kusafirishwa nje ya nchi.

Ngozi ghafi zinaweza kusindikwa na kuwa bidhaa zenye thamani kubwa zaidi kama viatu, mikoba, mikanda, samani na bidhaa nyingine zinazohitajika katika soko la ndani na la kimataifa.

Mtafiti Dk. Cecilia akisisitiza jambo wakati akizungumzia mafanikio ya utafiti alioufanya.

...............................

Dk. Cecilia anajaribu kuweka sehemu ya suluhisho hilo ndani ya Tanzania kwa kuzalisha dawa ya usindikaji wa ngozi kutokana na malighafi inayopatikana nchini.

Ikiwa uzalishaji huo utafikia kiwango kikubwa cha kibiashara, manufaa yanaweza kuonekana katika hatua mbalimbali kwa wakati mmoja. Maganda ya korosho yatapata matumizi ya kiuchumi, wakulima watapata fursa mpya za kipato, viwanda vitapata malighafi ya ndani na fedha zinazotumika kuagiza bidhaa kutoka nje zitabaki katika uchumi wa taifa.

Takwimu zinaonesha umuhimu wa hatua hiyo. Mwaka 2024, Tanzania ilisafirisha nje tani 6,689 za ngozi ghafi zenye thamani ya Shilingi bilioni 8.06. Hata hivyo, usindikaji wa ndani unaweza kuongeza thamani zaidi na kuimarisha mapato ya taifa.

Muonekano wa chupa zenye Vimiminika vilivyoandaliwa na kiwanda hicho kwa ajili ya kutengenezea ngozi.

................................

Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC) tayari kimetambua sekta ya bidhaa za ngozi zenye thamani ya juu kuwa eneo muhimu la uwekezaji kutokana na uwezo wake wa kuongeza ajira na kukuza viwanda.

Kwa mtazamo huo, kazi inayofanywa na Dk. Cecilia haipaswi kuonekana kama uzalishaji wa dawa pekee, bali ni sehemu ya kujenga ikolojia ya viwanda inayounganisha wakulima, wafugaji, watafiti, viwanda na masoko ya kimataifa.

Dk. Cecilia ameonesha nia ya kujenga kiwanda kikubwa mkoani Mtwara kutokana na ukaribu wa malighafi ya korosho. Kiwanda hicho kinaweza kufungua nafasi za ajira kwa wanawake na vijana katika ukusanyaji, usafirishaji, uzalishaji, ufungashaji na shughuli nyingine za viwandani.

Mbali na Mtwara, Dk. Cecilia anaangalia pia uwezekano wa kuwekeza katika Kanda ya Kati inayojumuisha mikoa ya Dodoma, Singida na Tabora, ambayo nayo imeanza kuimarisha kilimo cha korosho.

Bidhaa kama mabegi, mikoba, pochi na nyinginezo zilizotengenezwa na kiwanda kinachomilikiwa na Dk. Cecilia zikioneshwa.

............................... 

Akizungumzia mafanikio waliyofikia Dk. Cecilia anasema siyo haba kwani walianza na mtaji wa milioni 20 lakini sasa wamefisha mtaji wa shilingi milioni100.

Dk.Cecilia aliongeza kuwa kwa kuwa ndiyo wanaanza uzalishaji kwa msimu uliopita walikusanya maganda ya korosho kilo 3000 ambazo walizitumia kwa msimu mzima lakini msimu mpya wa mwaka huu wanatarajia kuongeza zaidi ya hapo.

"Uzalishaji kwa msimu uliopita ulikuwa mzuri, changamoto kubwa tuliyonayo ni ya kusafirisha hayo maganda kutoka Mtwara kuyapeleka Arusha na ndiyo maana tunafanya jitihada za kujenga kiwanda,' alisema.

WAKULIMA WAONA FURSA MPYA

Mkulima Karimu Chipola kutoka Kijiji cha Mchichila wilayani Tandahimba anasema ubunifu huo umeongeza thamani ya zao la korosho kupitia matumizi ya maganda ambayo awali yalikuwa hayatumiki.

“Sisi wakulima tunashukuru sana kwa sababu tunaamini zao letu limeongezewa thamani na hivyo tunaweza kupata kipato kingine,” alisema Chipola.

Mdau wa kilimo cha korosho, Dk. Fotunatus Kapinga, anasema lengo la tafiti ni kuhakikisha zina manufaa kwa jamii.

“Utafiti uliofanywa na Dk. Cecilia umeonesha mafanikio makubwa na unaweza kumwezesha mkulima kupata faida zaidi kuliko kutegemea korosho pekee hasa baada ya zao hilo kuongezwa thamani kupitia utafiti huo,” alisema.

Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH) Dk. Amos Nungu, akiwa na Dk. Cecilia wakati wa mkutano na wanahabari.

...............................................

Kuhusu COSTECH ; Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH) ni mshauri mkuu wa Serikali ya Tanzania katika masuala yote yanayohusu sayansi, teknolojia, na ubunifu kwa ajili ya maendeleo ya kijamii na kiuchumi. Taasisi hii ilianzishwa kwa Sheria ya Bunge Na. 7 ya mwaka 1986.

Kupitia Serikali COSTECH imekuwa ikitoa rasilimali fedha kwa ajili ya kuwezesha ufadhili wa bunifu mbalimbali.

...........................

Kijana Mohamed Namkwacha anasema amepata ajira kupitia ukusanyaji wa maganda ya korosho yanayosafirishwa kwenda Arusha.

“Awali hatukujua kama maganda haya yana thamani. Baada ya kupewa elimu na Dk. Cecilia, niliona ni fursa na nikaanza kujishughulisha na kazi hii,” alisema.

Kwa upande wake, Mohamed Makusi anasema katika msimu uliopita walikusanya tani tatu za maganda ya korosho kwa kushirikiana na vijana 10, wakiwamo wanawake watatu.

“Tunapongeza watafiti na COSTECH kwa kuleta bunifu zenye tija. Tunaiomba Serikali kuendelea kusaidia tafiti hizi ziwafikie wananchi badala ya kubaki kwenye makabati,” alisema Makusi.

SINGIDA YAJIPANGA KWA UWEKEZAJI

Katibu Tawala wa Mkoa wa Singida, Dk. Fatma Mganga, alimpongeza Dk. Cecilia kwa ubunifu wake na kumkaribisha kuwekeza mkoani humo.

Alisema Mkoa wa Singida umejipanga kuimarisha kilimo cha korosho, hasa katika Wilaya za Manyoni na Itigi, na umeweka mazingira rafiki kwa wawekezaji katika sekta za kilimo na viwanda.

“Mkoa wa Singida una ardhi yenye rutuba, maeneo yaliyotengwa kwa ajili ya viwanda na miundombinu mizuri ya barabara. Tunawakaribisha wawekezaji kuja kutumia fursa hizi,” alisema Dk. Mganga.

Dira ya Maendeleo ya Taifa ya 2050 inalenga kujenga uchumi wa dola trilioni moja wenye ushindani na tija. Uchumi huo hautajengwa na mradi mmoja au kiwanda kimoja, bali na maelfu ya mawazo yatakayogeuzwa kuwa bidhaa, kampuni na viwanda.

Safari hiyo imeanza kupitia uwekezaji katika sayansi, teknolojia na ubunifu. Na wakati mwingine, mwanzo wake unaweza kuwa mdogo kama Shilingi milioni 20, lakini matokeo yake yakawa makubwa zaidi kwa taifa katika siku zijazo.

Muonekano wa Jengo la Makao Makuu ya Bodi ya Korosho Tanzania (CBT)

......................................

Kuhusu Bodi ya Korosho Tanzania

Bodi ya korosho Tanzania ni Taasisi ya Umma iliyo chini ya Wizara ya Kilimo iliyoundwa chini ya sheria ya Tasnia ya korosho Sura ya 203 Toleo la Mwaka 2023, inayoipa jukumu la usimamizi wa Tasnia ya korosho kwenye mnyororo mzima wa thamani kuanzia kwa mkulima hadi kwa mlaji wa mwisho.

Makala hii imeandaliwa na Dotto Mwaibale namba ya simu 0754362990

 

No comments

Powered by Blogger.