TARI NALIENDELE YAFUNDISHA TEKNOLOJIA YA UVUNAJI WA ZAO LA UFUTA
Mratibu wa programu ya zao la ufuta kitaifa wa Taasisi ya Utafiti wa Kilimo
Tanzania (TARI) Naliendele Joseph Mzunda akizungumza na waandishi wa
habari baada ya kutoa elimu ya namna bora ya uvunaji wa ufuta kwa wakulima .Na Mwandishi Wetu, Mtwara
WAKULIMA na wadau wa zao la ufuta nchini wametakiwa kuzingatia ubora kwa
kuanzia katika hatua za awali za kulima, uvunaji na utunzaji wa zao hilo ili
kuendana na mahitaji ya soko linavyotaka.
Hayo yalisemwa na mratibu wa
programu ya utafiti wa ufuta kitaifa na mtafiti wa zao la ufuta kutoka TARI
Naliendele Joseph Mzunda wakati akitoa elimu ya namna bora ya kulima na kuvuna zao
hilo kwa baadhi ya wakulima ambapo alisema kuwa wadau wa zao la ufuta lazima
waangalie kuwa linapofika mikononi mwao lipo katika hali ya usafi ili
kusitokee lawama kutoka kwa wanunuzi.
Aidha Bw Mzunda alisema kuwa
wanunuzi wa ufuta wamekuwa na vigezo maalumu vinavyowafanya kununua ikiwepo
ubora,rangi na Ladha yake huku akielezea
upekee unaopatikana kwenye ufuta unaozalishwa nchini ukilinganisha na
nchi nyingine.
Mtafiti wa zao la ufuta kutoka TARI Naliendele akitoa maelezo kwa wakulima
namna bora ya kuvuna na kukausha ufuta
Hata hivyo Bw Mzunda amewataka wakulima kutunza kiasi cha fedha kwa ajili
ya kununua mbegu zilizokuwa bora na kwa ajili ya pembejeo na viuatilifu ili
iwasaidie kutumia katika msimu unaofuata
wa kilimo cha ufuta.
Fatma Athumani na Aisha Wilson wakulima wa zao la ufuta kutoka Kata ya
Naliendele wamesema kupitia elimu waliyoipata kutoka TARI itawasaidia katika
kuandaa mashamba na namna bora ya kuvuna zao hilo tofauti na hapo awali
walivyokuwa wakilima.
Wakulima wa zao la ufuta wakionesha njia bora ya kuvuna zao hilo na kuutunza.


No comments