Header Ads

MBUNGE WA JIMBO LA MLALO AKUTANA NA WAKULIMA WA MKONGE KUTATUA CHANGAMOTO ZAO

Mbunge wa Jimbo la Mlalo Mhe. Rashid Shangazi (MNEC), (wa pili kulia  waliokaa) akiwa katika picha ya pamoja na wakulima ambao ni wanaChama Cha Ushirika wa zao la Mkonge Umba (UWAMU) , baada ya kusikiliza kero zao Septemba 18, 2024.

.................................... 

Na Mwandishi Wetu, Lushoto

Mbunge wa Jimbo la Mlalo Mhe. Rashid Shangazi (MNEC) leo amekutana na Chama Cha Ushirika wa zao la Mkonge Umba (UWAMU) akiambatana na Mkurugenzi wa Bodi ya Mkonge Tanzania Ndugu Saddy Kambona , Mrajisi Msaidizi wa Vyama vya Ushirika Mkoa wa Tanga Ndugu Henjewele John pamoja na Viongozi wa Idara ya Kilimo Halmashauri ya Lushoto walioongozwa na Ndugu George Medeye.

Mhe. Shangazi ameitisha kikao hicho kilichofanyika katika Shule ya Msingi Kwezigha Kata ya Mnazi kwa  lengo la kutatua changamoto zilizowasilishwa kwake na wadau wa mkonge Tarafa ya Umba hususani changamoto ya kukosekana mitambo ya kuchakata zao hilo ndani ya Ushirika katika kuongezea thamani, hatua ambayo itakuwa ikiongeza kipato chao.

Viongozi wamezungumza mambo mbalimbali kama ifuatavyo:-

1) MHE. MBUNGE SHANGAZI: Ameanza kwa kumkaribisha sana Mkurugenzi wa Bodi ya Mkonge Tanzania na kumshukuru kwa kukubali kufika Mnazi kupokea changamoto za wakulima ili kuzitolea ufafanuzi na majawabu.

Mhe. Rashid Shangazi aliendelea kwa kutaka taarifa ya kitakwimu ya idadi ya wakulima wa mkonge hadi sasa, ukubwa wa eneo la kilimo na hali ya uzalishaji kwa mwaka.

Mhe. Shangazi ameelekeza takwimu hizo zihuishwe haraka iwezekanavyo na kuhakikisha wakulima wa mkonge wanaingia katika Chama cha Ushirika kwa lengo la kuwa na nguvu ya uzalishaji na uuzaji wa pamoja kwa faida.

Vilevile, ameonyesha wasiwasi wake juu ya uimara wa Ushirika huo na kufahamishwa ni kweli Ushirika unakabiliwa na changamoto za uendeshaji hasa upande wa michango ya viingilio na ununuaji wa hisa ambapo kila mwanachama anapaswa kuwa na hisa 5 zenye thamani ya Shilingi 100,000/=.

Hii imepelekea Mhe. Mbunge kusimamia kuwekwa kwa maazimio yaliyoonekana mwisho wa taarifa hii. 

2) MKURUGENZI WA BODI YA MKONGE TANZANIA:- Akizungumza katika Kikao hicho, Mkurugenzi wa Bodi ya Mkonge Tanzania ndugu Saddy Kambona amepongeza jitihada za Mbunge wa Jimbo la Mlalo katika kutafuta namna ya  kuwainua wakulima wa Mkonge.

Kambona amezungumzia hatua mbalimbali anazofanya kutafuta mwarobaini wa changamoto za wakulima wadogo wadogo wa Mkonge. Jitihada hizo ni pamoja na:-

A) Imeundwa timu ya wataalamu kutoka Wizara ya Kilimo, vyuo vikuu, na Kilimanjaro Tools kuzunguka nchi nzima kukagua teknolojia inayotumika katika viwanda vya uchakataji wa Mkonge ili waunde mtambo wa bei nafuu wa kuchakata zao hilo kuwawezesha wakulima wengi kununua.

B) Imeundwa timu ya wataalamu kukutana na watu wa Benki (Bankers) kuona namna watakuja na utaratibu nafuu wa kuwakopesha wakulima wa mkonge kwa masharti nafuu tofauti na wakopaji kutoka Sekta nyingine.

C) Bodi kwa kushirikiana na Wizara ya Kilimo imeendelea kuhakikisha wakulima wanauza Mkonge wao kwa Bei nzuri kwa kutafuta masoko ya uhakika.

Mkugenzi wa Bodi ya Mkonge Tanzania ametaja fursa mbalimbali zilizoko katika zao hilo akisema,

(a) Mkonge ni zao linalofanya vizuri sana Katika kunyonya hewa ya Ukaa, hivyo inaangaliwa namna ya kuwanufaisha wakulima wa zao hilo kupitia Biashara ya Hewa ya Ukaa.

(b) Mabaki ya Mkonge yanatumika kuzalisha mkaa wa kupikia.

(d) Mabaki ya Mkonge ya yanaweza kutumika kuzalisha mbao za kutengeneza samani (furniture).

Mkurugenzi ameshuhidia  mabaki ya Mkonge katika Tafara ya Umba yakitupwa na kuchomwa moto, hivyo anafanya Kila liwezekanalo kuhakikisha yanawapatia fedha wakulima.

Hata hivyo, Mkurugenzi Kambona amesema pamoja na kwamba katani inahimili mazingira magumu na kame, ni muhimu mashamba ya zao hilo yatunzwe kwa kulimiwa na kutochoma moto ili uzalishaji uongezeke. Amesema wenzetu China wanapata mavuno makubwa karibu mara 4 zaidi ya Tanzania kwakuwa walima mashamba yao na kuyatunza wakati wote wa ujuaji hadi hatua ya kuvuna.

Ameongeza kuwakumbusha wakulima kwamba uvunaji wa Mkonge ufanyike Kila baada ya mwaka 1 badala ya uvunaji unaoendelea sasa ambao majani yamesimama wima hayasubiriwi yakitanua.

Aidha, wakulima wa Mkonge wameaswa kuzivumilia changamoto za sasa za uzalishaji wa zao hilo akisema kupitia mipango na jitihada zinazofanywa na Bodi ya Mkonge na Wizara ya Kilimo ni dhahiri mazuri yanakuja hivi karibuni kwani maelekezo ya Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ni kuhakikisha Kilimo kiinakuwa na tija kwa Mkulima na Taifa.

3) MRAJISI MSAIDIZI WA VYAMA VYA USHIRIKA TANZANIA:- Ndugu Henjewele wakati akitoa mafunzo kwa wakulima na kueleza faida za Vyama vya Ushirika amesema Chama cha Ushirika kinaundwa na ngazi tatu ambazo ni:- 

1. Wanachama,

2. Bodi ya uongozi - yenye wajumbe kuanzia 5 hadi 9 wanaotokana na wanachama hao, na

3. Watendaji - ambao wanaaajiriwa na Bodi.

Kama Ushirika ukiyumba ni matokeao ya Malindi yayo matatu kutotimiza wajibu wake ipasavyo. 

Ndugu Henjewele alewela wazi utayari wake kurudi tena Tarafa ya Umba kutoa Elimu zaidi kwa wakulima katika Ushirika wa UWAMU.

4) AFISA KILIMO WA HALMASHAURI (W) LUSHOTO:- Afisa Kilimo wa Halmashauri ya Wilaya ya Lushoto ndugu George Medeye amesema uzalishaji wa zao la Mkonge katika Tarafa ya Umba unaongezeka kwa kasi kubwa sana kwa kila mwaka kwani mwaka uliopita 2023 uzalishaji ulikuwa zaidi ya Tani 1,200 wakati mwaka huu 2024 matarajio ni kuvuna  zaidi ya kiasi hicho ikizingatiwa kwamba kufikia mwaka 2024 Mkonge uliofikia hatua ya kuvunwa ni Hekta 2,000 sawa na Ekari 5,000.

Ameongeza kusema idadi ya wakulima wa Mkonge mwaka 2023 ilikuwa 500, takwimu zitakazokusanywa mwaka huu zitakuwa na ongezeko kubwa sana.

Medeye ameahidi kuyafanyia kazi maelekezo yote ya Mkurugenzi wa Bodi ya Mkonge Tanzania, Mhe. Shangazi pamoja na Viongozi wengine kuhakikisha baada ya muda mfupi Mkonge unawatajirisha wakulima.

5) MENEJA BENKI YA CRDB LUSHOTO:- Meneja wa Benki ya CRDB ndugu John Mtani amezungumza na wakulima katika Ushirika wa Mkonge UWAMU kuwatangazia fursa mbalimbali zinazopatikana katika Benki yao akitolea mfano wa huduma za mikopo ya  Fahari Kilimo na Imbeju.

Mtani amesema sifa mojawapo ya Ushirika kukopeshwa na Benki ya CRDB ni kuwa na Akaunti ya Benki hiyo.

Ameendelea kusema Benki ya CRDB inatoa fursa kwa wakulima kufungua Akaunti ambazo hazina gharama ya uendeshaji. Hivyo CRDB ni Benki inayojali Malindi mbalimbali bila kusahau wakulima wa Mkonge.

6) MAKAMU M/KITI WA UWAMU:- Ndugu Abdallah Kumbi ameeleza furaha yake kutokana na yote yaliyowasilishwa na Mhe. Rashid Shangazi Mbunge, Mkurugenzi wa Bodi ya Mkonge Tanzania, Mrajisi wa Vyama vya Ushirika Mkoa wa Tanga, pamoja na Viongozi wengine akisema awali alikuwa akiwalaumi viongozi hao kwakuwa alikuwa anakosa taarifa sahihi na mipango mizuri iliyowasilishwa katika kikao.

Ndugu Kumbi Abdallah ameahidi kutoa ushirikiano kwa Mhe. Mbunge na viongozi wote kuelekea katika mabadiliko makubwa ya Ushirika na Uzalishaji wa Mkonge.

7) MENEJA WA UWAMU:- Ndugu Bakari Huseni Sefu amesema ushirika wa UWAMU umepata nafasi kutembelea vyama vya Ushirika wa Mkonge Magoma - Korogwe na kubaini wenzao wakiwa na mafanikio Makubwa sana kiasi cha kuuaga umasikini.

 

MAAZIMIO YA KIKAO:

Miongoni mwa maazimio ya kikao ni pamoja na:-

(1) Kila mwanachama wa UWAMU akamilishe malipo ya Tsh. 10,000/= ya kiingilio cha kujiunga na Chama kabla ya Desemba 2024.

(2) Kufungua Akaunti katika Bank ya CRDB kwa ajili ya kuongeza wigo wa kukopesheka.

(3) Kukamilisha taarifa ya sasa ya idadi ya wakulima wa Mkonge, idadi ya Hekta zinazolimwa Mkonge na kiasi cha uzalishaji kwa mwaka.

(4) Kila Afisa Ugani katika Tarafa ya Umba awe anajishughulisha na Kilimo cha Mkonge kama shamba darasa kwa wengine na awasilishe ripoti ya uzalishaji wake.

(5) Afisa Kilimo Wilaya afuatilie swala la mashine ya kuchakata Mkonge kwa mwekezaji aliyeahidi kusaidia mashine moja.

(6) Afisa Kilimo Wilaya aandike andiko kwenda kwa Mkurugenzi wa Stakabadhi Ghalani kuomba ghala la kuhifadhia Mkonge (Warehouse) Tarafa ya Umba.

(7) Afisa Kilimo Wilaya ashirikiane na Diwani wa Mnazi kutafuta eneo la Ghala la Mkonge ndani ya Kata ya Mnazi.

(8) Ushirika wa UWAMU Kufanya mkutano kila baada ya miezi 03 badala ya Mkutano 01 unaoelekezwa kwa mujibu wa Sheria. Lengo ni kuharakisha kuimarika kwa Ushirika huo na utekelezaji wa haraka wa maazimio. Hivyo kutakuwa na kikao mwezi Desemba, 2024.

Mhe. Mbunge amehitimisha kwa kumshukuru Mkurugenzi wa Bodi ya Mkonge Tanzania ndugu Saddy Kambona kwa utayari wake mkubwa kuwasaidia wakulima wa Mkonge Kupitia Chama cha Ushirika UWAMU.

Vilevile, Mhe. Mbunge amewashukuru wakulima wa Mkonge kwa kushiriki kikao hicho kuwasilisha kero zao na  kupokea yale yaliyowasilishwa na viongozi kutoka juu.

Kubwa zaidi, Mhe. Rashid Shangazi amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuipa uhai mkubwa Wizara ya Kilimo katika uzalishaji na masoko chini ya Waziri wake Mhe. Hussein Bashe.

 

No comments

Powered by Blogger.